Tuesday, January 13, 2009

LISHE MUHIMU KWA MWANAMKE KUPATA UZAZI

Tmeshasikia ndoa nyingi zikiingia kwenye migogoro kwa kukosa mtoto kutokana na kila mmoja kumshutumu mwenzake kuwa ndiye chanzo. Inatokea mume anataka mtoto lakini mke hana uwezo wa kushika mimba au mke anataka mtoto lakini mume hana uwezo wa kumpa ujauzito mke.

Inawezekana kukawa na sababu nyingine nyingi za kitabibu zinazosababisha mwanamke kukosa uwezo wa kuzaa (infertility), lakini wakati mwingine sababu huwa ni ukosefu wa baadhi ya virutubisho vinavyosaidia kupatikana kwa mayai ya uzazi, ambavyo vinatokana na vyakula tunavyokula kila siku.

Kwa mwanamke mwenye matatizo ya uzazi, makala ya leo yaweza kuwa na msaada kwake, tunaeleza vyakula vinavyopaswa kuliwa na vinavyopaswa kuepukwa ili kujiweka katika nafasi nzuri ya kupata uzazi:

Lishe ni sehemu muhimu ya mwanamke kupata mayai ya uzazi na lishe hiyo inatakiwa iwe ya vyakula vya aina mbalimbali vya asili ambavyo ni pamoja na vyakula vyote vitokanavyo na mbegu (mahindi, mtama, njegere, maharage, ufuta, n.k) vikiambatana na maziwa yenye kiasi kidogo cha mafuta (fat free milk).

Vyakula vingine ni mboga mboga, matunda pamoja na karanga, korosho, asali na mafuta yatokanayo na mimea (vegetable oils) na siyo mafuta mengine ambayo huongeza kolestro mwilini.

Asilimia 70 hadi 80 ya vyakula utakavyokula katika mlo wako wa kila siku, viwe vya asili na ambavyo huliwa bila kupikwa, kwani upikaji wa vyakula nao huchangia kwa kiasi fulani kupunguza virutubisho kwenye vyakula. Hivyo matunda ya aina mbalimbali, korosho, karanga, n.k viliwe kwa wingi.

VYAKULA VYA KUEPUKWA
Wakati ukizingatia ulaji wa vyakula vilivyosisitizwa hapo awali katika mlo wako wa kila siku, epuka kula vyakula vyenye mafuta mengi na vilivyoungwa kwa viungo vingi vya aina mbalimbali. Epuka kunywa chai na kahawa kwa kiasi kingi, unapokunywa sharti uweke kiasi kidogo sana cha kahawa au chai.

Vyakula vingine vya kuepukwa ni pamoja na sukari nyeupe badala yake pendelea ‘brown sugar’. Epuka vyakula vilivyotengenezwa kutokana na unga mweupe, nyama nyekundu, vyakula vya kukaanga au kupikwa kwa mafuta mengi.

Ushauri mwingine unatolewa kwa wanawake wenye tatizo la uzazi ni pamoja na kusafisha mwili uondokane na sumu kwa njia ya kufunga kwa siku mbili hadi tatu.

No comments: